







Tigo Tanzania imetangaza uzinduzi wa Muziki wa Tigo ujulikanao kama “Tigo Music” kwa kushirikiana na Deezer, ambayo ni huduma ya kimataifa inayorusha muziki itakayowapa Watanzania muziki usiokuwa na kikomo.
Akizindua huduma hii mpya, Meneja Chapa wa Tigo, William Mpinga, alisema kuanzia Januari 24, wateja wa Tigo wenye vifurushi vya malipo ya kabla ya intaneti wana uwezo wa kupata nyimbo milioni 36 za wasanii wa Kitanzania na Afrika kwa ujumla katika simu zao za mkononi za smartphone.
Vilevile, Tigo itatafuta miziki mipya ya kusisimua ya wasanii wa ndani kupitia ushirikiano mpya na kampuni ya Africa Music Rights, ambayo inawezesha, kutafuta na kusimamia haki za muziki katika bara la Afrika, alisema Mpinga.
Kutakuwa na ghafla ya uzinduzi kwa ajili ya Tigo Music katika viwanja vya Leaders Club Dar es Salaam tarehe 24 Januari ambapo wananchi watatumbuizwa na nyimbo tofauti tofauti kutoka kwa wasaniii wa hapa nchini kama Diamond Platinum, Ali Kiba, Professor J, Vanessa Mdee, Ben Paul, Isha Mashauzi, Malaika Band, Khadija Kopa, Yamoto Band, Msondo, Sikinde na wengineo.
Juu ya kuwapa wateja wa Tigo uwezekano wa kupata miziki ya kimataifa na ya hapa nchini bila kizuizi chochote, Tigo Music, itawapa nafasi wasanii wa hapa nchini kujiongezea kipato kutokana na nyimbo zao ambazo zitakuwa zimesikilizwa kupitia huduma hii. Tigo itawapa wasanii hawa mafunzo ya jinsi ya kutumia na kunufaika na huduma hii, alisema Bwana Mpinga.
“Kampuni ya Tigo Tanzania ni kampuni iliyojengwa juu ya msingi imara wa ubunifu. Tunafurahia kuwa kampuni ya kwanza ya mawasiliano Tanzania kuwapa wateja wetu muziki usiokuwa na kikomo”.
“Kama bidhaa yenye maisha ya kidijitali, lengo letu ni kuiwezesha tasnia ya muziki kwa kujenga jukwaa ambalo si tu linaruhusu kupata nyimbo za wasanii wa ndani kwa urahisi, lakini pia linawapa mafunzo wanamuziki wetu kwenye masuala muhimu kama vile haki miliki na masoko. Hii ni njia yetu ya kusaidia vipaji vya wasanii na kukuza tasnia ya muziki wa ndani, “aliongeza.
Tigo itaanzisha vifurushi mbalimbali vya huduma ya muziki ambavyo vitawawezesha wateja wake kuvipata moja kwa moja kupitia * 148 * 00 #.
Kuanzishwa kwa Muziki wa Tigo (Tigo Music) nchini Tanzania kumetokana na mafanikio ya uzinduzi wake nchini Ghana mwaka 2014 na Amerika ya Kusini mwaka 2012. Tangu kuanzishwa kwake imekuwa ni sehemu muhimu kwa maisha ya kidijitali ya watu ya kila siku na hii inaendana na matukio ya muziki wa ana kwa ana yaliyowahi kufanywa na wanamuziki mashuhuri duniani, pamoja na yale yaliyorekodiwa ndani ya studio.
Urushwaji wa muziki ni eneo linalokua kwa haraka sana katika tasnia ya muziki kimataifa, na bidhaa ya muziki tayari imekuwa ya pili kimaarufu kwenye vipengele vya simu za mkononi katika Afrika.